Ni HISTORIA ILIOJEE! mwanamke jasiri, shujaa na mwenye msimamo, moja ya barabara kuu ndani ya jiji la Dar es Salaam, jina lake limo kwa heshima ya mchango wake mkubwa wa kuleta uhuru wa Tanganyika.
Si mwingine ni Bibi Titi Mohamed, mwanamama, aliyekuwa kiongozi mmojawapo katika harakati za kudai uhuru wa Tanganyika, baadaye aliongoza Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT), chama cha wanawake katika chama cha Tanganyika African National Union (TANU), na baadaye akawa waziri wa wanawake na masuala ya kijamii katika serikali ya Mwalimu Nyerere.
Bi Titi Mohamed alikuwa mwanamke wa Kiislamu aliyezaliwa jijini Dar es Salaam mnamo mwaka 1926 na baba mfanyabiashara na mama mkulima. Alipata elimu ya shule za msingi pekee na alipofikisha umri wa miaka 14 tu aliolewa na mume mzee.
Bi Titi Mohamed alipata nguvu ya kuwa mwanaharakati kupitia kipaji cha kuimba, enzi za ujana wake alikuwa mwimbaji mzuri wa kwasida na hivyo kuwa kama mwimbaji kiongozi katika ngoma katika kikundi cha muziki na ngoma ambacho kilimwongozea uzoefu wa kuwa mbele ya umati.
Nguvu ya kushiriki katika majukumu ya uongozi na uhusiano ndani ya mitandao wanawake na mapambano ya kitaifa yallianza mwaka 1950, baada ya Vita Kuu ya II ya dunia, Tanganyika ikiwemo nchi nyingine katika harakati za uzalendo zilikuwa zimeshika kasi. Mwaka 1954, TANU iliundwa chini ya uongozi wa mwalimu na baadaye Rais Julius Nyerere.
 |
Bibi Titi na Mwalimu J.K Nyerere kwenye pozi enzi hizo |
Muda si mrefu baadaye mwaka 1955, Bibi Titi alikasimishwa kiti cha UWT, na ndani ya miezi mitatu ya uteuzi wake, walijiunga wanawake zaidi ya 5,000 kama wanachama wa TANU, na hivyo kwa mrengo huo wa wanawake uliianzishwa na jukumu kubwa kwa mapambano ya uhuru na UWT kufanya kazi kubwa ya kukuza maadili ya TANU kwa raia. Pia umoja wanawake ukapaza sauti moja katika mapambano dhidi ya ukoloni.
Bibi Titi kupitia wanaharakati wanawake walikuwa na uwezo wa kutumia mitandao yao mbalimbali ya kijamii na kiuchumi kwa kuongeza fedha kwa kiasi kikubwa kwaajili ya chama cha TANU. Zaidi ya hayo, Bibi Titi akiwa na kipawa cha usemaji, yeye mwenyewe, alihamasisha wanawake kupitia makundi ngoma na kusimamia viongozi wao kuunda nafasi kwa ajili ya kushughulikia wanachama na kuwasaidia, pia makundi hayo yalikuwa wazi kwa wanawake wote waliotaka kujiunga, na kuishia kuwa mitandao yenye nguvu kisiasa ajili ya kubadilishana taarifa, tangazo la mikutano ya kampeni na maandamano.
Mwishowe mafanikio yaliingia mwaka 1961, kwa Tanganyika kupata Uhuru.
Bibi Titi Mohamed bahati mbaya kisiasa ilimpata mwaka 1965 wakati alipopoteza kiti chake cha ubunge. Mwaka 1967, yeye alijiuzulu kutoka uwaziri .
Baadaye alipata masaibu ya kisiasa kwa kiasi kikubwa ilifanya kutoweka katika maisha ya umma na baadaye mnamo Novemba 5, 2000, Bibi Titi Mohamed pumzi yake ilirejea ilipotoka katika hospitali ya Net Care huko Afrika Kusini.
HISTORIA ILIOJEE inajivunia Bibi Titi, mwanamama wa shoka, malkia wa nguvu atakumbukwa kwa mengi, heshima yake ipo kwenye kutoa mwanga wa harakati za wanawake dhidi ya mfumo mibovu kwenye kila nyanja ya maisha, kwetu sisi WAUNGWANA ni HISTORIA ILIOJEEE!